-->

Chriss Mhenga Chimbuko Bongo Movie (Sehemu ya Pili)

Inaendelea ilipoishia …..
Na bado anaamini kuwa makundi ndio kila kitu kuliko kumchukua msanii moja huku mwingine kule kwani kila mtu anavyokuja anakuja kwa ajiili ya kazi hiyo tu hana muda wa kumsikiliza mtayarishaji au muongozaji vitu vingine vya ziada, watarekodi na kusambaratika hadi kazi nyingine.

Mhenga kazini

Sanaa ni taaluma ni lazima wasanii kila siku wawe na muda wa kujifunza kwa aina ya kuwakusanya na kufanya kazi wasanii wanakuwa hawana kitu kipya kila siku ni wale wale wasiojua kitu zaidi ya kuwa na filamu nyingi ambazo hazina kitu cha kukumbukwa.

“Siku hizi wasanii hata hawatumii script wanategemea kuitwa tu na kuambiwa na mwenye sinema njoo na nguo zako nne anaambi wa utasema hivi hivi na akacheza scene zake tano akapewa laki mbili siku hiyo hiyo,”

“Hivi kwa staili hiyo unafikiri kuna msanii atakumbuka kurudi shule kweli na pesa anapata kirahisi hivyo atakwambia wewe somea hiyo filamu sisi tunatengeneza pesa huku,”

“Katika sanaa si urembo wa mtu tu, si kwa mapenzi ya mtayarishaji kuwa kamuona mtu sanaa ni kitu kingine kinaenda mbali zaidi ni taaluma wasanii wanapata pesa kirahisi ndio sababu ya dharau,”
Mwigizaji anaona kuwa kumbe ni kazi rahisi sana ambayo anaenda mara siku moja tu na kujipatia fedha hapo ndio suala ukosefu wa nidhamu linaanzia hapo na tatizo lingine watayarishaji wanathamini waigizaji kuliko hata muongozaji jambo ambalo linawafanya wasanii kuwa waongozaji japo hawana taaluma hiyo.

JUHUDI ZA KURUDI WASANII WA KAOLE ZILIGONGA MWAMBA?
Kulikuwa na juhudi za makusudi kutaka kuwakusanya wasanii waliokuwa na nyota kwa wakati wa kundi Kaole Sanaa Group lakini kimya, Mhenga anakiri kweli lilikuja kundi na kupewa jina la Kaone Group lakini hajui limekwama wapi na yeye hawezi kuongelea hilo si kiongozi wake.

“Siwezi kuongelea hilo maana sijajua kufa ni kwa maana ya kutoonekana katika Televisheni, lakini ninachojua kundi bado lipo labda tu ratiba zao za kukutana ndio mimi sizijui,”

Kuzaliwa kwa kundi la Kaone ilikuwa juhudi za msanii Issa Kipemba yakaibuka malumbano ya matumizi ya jina lakini baada ya marekebisho wakasajiliwa na kupata kituo Tv 1, baada ya hadithi ya Kipusa ya Kipemba kurefushwa na kuwa ya tamthilia badla ya filamu na huu ndio ulikuwa mwisho wa kukutana nao.

Mhenga akirekodi filamu

JE ANAONGELEAJE KUHUSU UBORA WA KAZI ZETU?
Watayarishaji wanasema kuwa filamu zao za ndani hazina ubovu wowote bali zinahujumiwa na filamu kutoka nje ya nchi lakini si kweli kama mbovu lakini mtaalam huyu anakiri ulipuaji katika utengenezaji wa kazi za ndani wala si utumiaji wa vifaa vya kisasa kama Kamera au teknolojia ya ajabu.

Utengenezaji wa filamu unategemea sana hadithi itakayoweza kuwakilishwa na mhusika mwenye ujuzi wa utengenezaji na si vingenevyo, mlaji ambaye ni mtazamaji anaangalia ni hadithi inayomgusa na kuonyesha maisha yanayomzunguka bila hivyo hawezi kununua.

“Mtazamaji anaangalia utampatia kile anachotarajia je ni stori ambayo inaweza kumkamata mtu na kuona kuwa ni sehemu yake aua ndio unashindwa kusimulia,”

Hadithi za filamu kwa sasa anaamini hazina nguvu lazima kuwe na nafasi za waongozaji, wasanii nao wana nafasi zao bila kusahau waandishi wa miswada haiwezekani kila siku msanii anakuwa na mwandishi mmoja tu katika kuandikiwa sinema tena mwandishi asiye na ujuzi lazima kazi mbaya zitokee.

Japo anakiri kuwa pamoja na kuwa na vifaa vya kisasa wazungu pia wanatengeneza filamu mbovu baadhi ya kazi zao unaweza kuangalia na kupitiwa na usingizi lakini kwetu tumezidi kutengeneza kazi mbovu zisizo na viwango.

Ubovu wa hadithi zetu unatokana na waandishi wa miswada kuandika tu bila kufanya utafiti mtazamaji akiona tu anaona mwandishi kabuni tu, hadithi ambayo imejaa mashaka makubwa na kumkimbiza, Mhenga anasema yeye ni muumini wa Weledi lazima watu warudi shule wasomee filamu.

Anatolea mfano wa filamu za Ukimwi zipo nyingi lakini bado inaweza kuja taasisi na kukupa kazi ya kutengeneza kazi nyingine huwezi kusema zipo nyingi lazima ufanye utafiti na kubuni njia ya kutengeneza kitu cha kipekee kitakachokubalika, kwani maana ya Kipaji ni utofauti wa kufanya kitu.

Ukosefu waandishi wa Muswada anaamini ni tatizo kubwa sana kwani waandishi waliopo hawana uwezo wa kuandika vitu vya kudumu na kukumbukwa wanafanya ubabaishaji katika uandishi na kusababisha uzalishaji wa kazi mbovu ambazo hazina ubora.

Pamoja na kuwa na uwezo wa kuandika anashauri mwandishi kuwapatia waandishi wenye weledi na fani hiyo kupitia na kutoa maoni yao inaweza kusaidia kupata kazi nzuri kuliko kujiamini na kufanya kazi kwa kulipua kwa watayarishaji kung’ang’ania waandishi wabovu ndio sababu ya tasnia kuyumba.

Mwandishi anatakiwa kwenda na wakati pia kuangalia matukio mapya, kutambua utofauti wa tamaduni, mila na desturi katika jamii inayowazunguka watanzania, kwani anaangalia mafanikio katika tamthilia ya Dhamira anayoifanya na kuruka katika runinga ya ITV mrejesho ni mkubwa.

Anajaribu kuongelea changamoto ya elimu ya Tanzania na maisha halisi ya walimu wa shule zetu, kupitia tamthilia hiyo mijadala mikubwa imeibuka kuhusu vitabu vya shule vinavyotumika katika kufundishia vikiwa na makosa ya wazi, amepigiwa simu hadi na baadhi ya wanazuoni wakubwa wakimpongeza.

Tamthilia anayoitayarishaji na kuiongoza limekuwa ni jukwaa kubwa la wanajamii viongozi wakubwa wakifuatilia jinsi gani anavyoibua mambo ambayo hata wanasiasa wanaweza kuyasahau na kulipoteza Taifa kama wanafunzi wa daraja moja wanatumia vitabu tofauti tutegemee nini baadae katika Taifa letu?

“Sisi kama Watanzania tuna maadili yetu lazima ujue watu wako mfano ukiangalia Dhamira unaona jinsi mwalimu anavyowakilisha mawazo ya walimu na kupokelewa vizuri na walimu wenyewe,”

JE MSANII WAKE BORA NI YUPI?
Uncle Chriss anakiri kwa kusema kuwa anashindwa kusema kukwepa hilo na atakuwa mkweli tu, kama angeambiwa asema mwigizaji bora kwa waigizaji wa kiume ni marehemu Steven Kanumba hakuna mwingine kwani pamoja na umaarufu wake hakujikweza kwake kila alifika kuchukua ushauri kwake.

“Kanumba kaondoka lakini alikuwa na kitu cha kipekee nidhamu, baada ya kuondoka yeye hakuna bora kama yeye na kwa upande wa kike Yvonne Charryl (Monalisa) ndio mwigizaji bora,”

Mhenga anasema kuwa pamoja na kuwa Monalisa si mwigizaji aliyetoka mikononi mwake lakini kwake anaona ndio mwigizaji bora wa kike wa karne kwani ameshakutana naye katika kazi chache lakini uwezo wake ni wa juu sana kuliko mwigizaji mwingine wa kike Tanzania.

Na amekuwa akikua kila siku badala ya kushuka katika tasnia ya filamu tofauti na wasanii wengine ambao pamoja na kutokudumu lakini wamejaa ujivuni katika tasnia ya filamu pamoja na kuwa hawajui kitu kwenye fani hiyo ambayo inahitaji kujifunza kila siku kulingana na ukuaji wa teknolojia.

Chanzo:Filamucentral

Comments

comments


Unataka kutangaza nasi? Tumia namba ya simu hapo chini.

Please contact us: email : info@bongomovies.com or Mobile: +255 756 348 364