-->

Maoni:Darassa Kazimwa na Rais Magufuli…

255 champion boy niite Mbwana Samatta haaa…” Ngoma linaanza kibabe. Linaisha kindava. Na ‘biti’ ya kikatili kama sound track ya movie la kimafia. Lazima ukae.

Darassa

Alikuwa yeye tu kwa kipindi kirefu. Aliwafunika wanamuziki wote mpaka mashabiki wao. Miaka mingi imepita bila wimbo wa kutikisa nchi hii kutoka. Darassa alipokuja na ngoma yake ya “Muziki” alishitua watu na wanamuziki wenzake.

Kadiri muda ulivyokwenda ndivyo vituko vilizidi kuongezeka kupitia wimbo wake.

Achana na yule dereva huko Singida aliyeachia usukani gari ikiwa kasi kwa sababu ya mizuka ya wimbo wa Darassa. Hapo kati yalitokea ya kutokea. Totoz mitandaoni zilijirekodi zikiucheza muziki wake. Ilivutia sana.

Hata maneno kwenye wimbo yake yakageuka misemo mitaani. Ni maneno ya kila siku lakini wimbo huu ni kama ulifufua vinywa vya watu kuyatumia.

Bampa to bampa. Ni kama yale ya Nature ya “Weka kigingi niweke jiwe, weka ugoko niweke chuma”.

Ni maneno yanayotumika sana kwa watu wa mpira viwanjani na mitaani. Yapo sana ila kwa utamu wa wimbo wake yakawa kama maneno mapya.

Wimbo ulipendwa na watoto wazee na zaidi vijana. Na kilichotia chumvi zaidi ni watoto wazuri wa mjini kujirekodi wakiucheza na kutupia mitandaoni, ilizidi kunogesha utamu wa wimbo.

Ungetamani kumuona Lulu alipojirekodi akiucheza wimbo huo, kwa namna ya pekee akifuatisha midundo na maneno kwa maringo. Ilivutia.

Na ungedata na Jokate, naye alijirekodi kwa namna ya kujidekesha kama mtoto mdogo anayefundishwa kuucheza. Ilitia raha kumtazama.

Kuna binti mzuri zaidi na mdogo zaidi ambaye alijirekodi ndani ya duka la nguo. Kila mwanaume mkware mitandaoni alitamani kumfahamu yule binti.

Umbile lake sura na namna alivyokuwa akiufuatisha wimbo huo uliwachanganya akili. Hasa pale anaposema “Waote mapembe waongezee mkia”.

Kila mtu alimuongelea Darassa na wimbo wake. Ni kama ulikuwa wimbo wake wa kwanza kumbe ana nyimbo kibao kabla.

Ndiye mwanamuziki pekee ambaye alipita katikati ya msitu mzito wa Diamond na Kiba. Akapasua na kuwaacha wakiwa hawaamini kinachotokea. Ikawa ngumu sana watu kusikiliza wimbo mpya.

Ujio wake lilikuwa pigo kwa Ommy Dimpoz na “Kajiandae” akiwa na Kiba. Rich Mavoko na “Kokoro” akiwa na Diamond. Mwana FA na “Dume Suruali” akiwa na Vanessa Mdee.

Wote hao nyimbo zao zilizimwa ghafla. Wakatoweka.

Masikio ya Watanzania yalielekezwa kwa Darassa. Bila Darassa wimbo wa FA “Dume suruali” ungekuwa habari ya mjini. Hata Dimpoz na Mavoko walikuwa na ngoma kali wakiwa wamewashirikisha miamba mikubwa. Lakini haikuwasaidia kuepuka kikombe kichungu cha Darassa. Ulikuwa wimbo wa Taifa unaoanza kindava. Unaisha kibabe. Na mdundo ni wa kikatili. Lazima unyooshe mikono juu.

Kama una roho nyepesi unaweza kulisusa na game lenyewe la muziki. Ujio wake kwenye wimbo huu hauna tofauti na ule ujio wa marehemu Ngwair na “Mikasi”. Ferouz na “Starehe”. Profesa Jay na “Ndiyo Mzee”. Nature na “Sitaki demu”.

Hapo katikati ulipita muda mrefu bila kutoka wimbo wa kushitua watu na kusambaa kwenye mioyo ya watu wa rika zote mpaka balaa la Darassa lilipotua kama bomu la nyuklia mwaka jana.

Ukatili aliofanya kwa wanamuziki wenzake hauna tofauti na ule wa Inspector Haroun na “Mtoto wa Geti Kali”. Watu walitaka kumsikiliza Inspector kila wakati kuliko taarifa ya habari.

Darassa baada ya wimbo wake huo, alichoshwa na safari kwenda kwenye shoo. Alikerwa na simu yake kwa mapromota na waandishi. Akaumizwa bega kwa ‘hagi’ za mashabiki hasa totoz.

Wanawake wepesi kutoa heshima kwa mtu maarufu kwa salamu au kuomba kupiga naye picha. Tofauti na wanaume wanapenda kukaza bila sababu ya msingi hasa Wabongo wanapokutana na staa.

Kila kona ni Darassa. Lakini hii leo unamsikia tena Darassa? Ni rahisi kumsikia Harmorapa kuliko yeye. Muda hauna fadhila na mtu. Muda wa wimbo wake umeshapita. Leo hii Nay Wa Mitego ndo kitu kinachoendelea kwenye vinywa vya watu.

Kama zali tu, wimbo wa kawaida. Maneno ya wimbo huo ndo tunayoyaona kwenye post za watu mitandaoni.

Wakati watu wakifurahia comments na likes za watu mitandaoni. Yeye alichofanya ni kuchukua maneno hayo akayatengeneza kwenye mtindo wa mashairi, midundo na kutiririka nayo. Kitu kimeitika.

Hafurahii likes na comments kama za wale wa mitandaoni. Ila anachekelea pesa anayoingiza kupitia wimbo huu.

Ukitaka ‘stress’ za kujitakia kwa sasa, fanya shoo moja na Nay. Shangwe atakazopata unaweza kutamani kuacha muziki na kufanya shughuli za kilimo na ufugaji.

Masikio ya Watanzania wanataka kusikia kile alichoimba Nay. Huu siyo muda rafiki na nyimbo za kubembelezana kimapenzi. Serikali yenyewe haibembelezani na mtu. Ni kanyaga twende siyo muda wa ‘Ala za Roho’ na kina Diva.

‘Dai’ na Kiba wakomae kimataifa tu. Kwa sasa muziki wa Bongo unataka kile alichofanya Nay. Huu ni mwanzo tu kuna mipini kibao inakuja.

Watu walikuwa wanasubiri tobo wazame. Alianza Darassa kila mtu mpenzi wa muziki aliona kwamba Hip Hop imerudi kupitia akili ya Darassa, sasa kuna Nay naye kadondosha fataki. Subiri mabomu zaidi na mkuu karuhusu watoto wa ‘kihuni’ wafanye kile roho inataka kwa sasa. Kama Nay alichosema kichaa kapewa rungu.

Ni kama fisi aliyekutana na mzoga. Kuna kundi la ‘wahuni’ wanapishana kwenye milango ya studio kuandaa ngoma. Unadhani wimbo wa Darassa “Muziki” ulikuwa bora kuliko nyimbo zake zote alizowahi kutoa? Usijidanganye, unaweza kuwa ndo wimbo wake wa kawaida ambao hakutumia akili nyingi na muda mrefu kuandaa. Ni wakati tu na ukifika hakuna wa kuzuia.

Watu walichoka na mwendelezo wa watu wawili tu kila siku ndiyo ukweli. Masikio yalikuwa yanataka kitu kipya tatizo waliokuwa kwenye mtiririko hawakuweza kufanya kitu bora zaidi ya wawili hao.

Darassa akaja kuvunja mwiko kibabe. Ndivyo ilivyo kwa Nay. Wimbo wake wa “Wapo” siyo bora sana kuliko nyimbo ambazo amewahi kutoa huko nyuma ila katoa kitu muafaka kwa wakati muafaka. Mwache apige pesa. “Wapo” ndo kitu pekee kinachosikilizwa kwa sasa Tanzania.

Siyo kwamba “Wapo” ni bora sana kuliko “Muziki” yawezekana “Muziki” ukawa bora zaidi ila wakati hauna ndoa na mtu.

Nay kapata zari kubwa na ni miongoni mwa Watanzania wenye bahati kubwa na utawala wa Magufuli kwa kilichotokea.

Kazi ngumu sana katika sanaa ya muziki inayochukua muda na pesa kuifanya, yeye imefanyika ndani ya saa 24 tu.

Promo ya wimbo kwa sasa si jambo dogo, ila Mheshimiwa Mwakyembe na Rais Magufuli wamemrahisishia kazi huyu Mchagga nusu na Mnyakyusa.

Wimbo wake ungepita tu kama upepo wa feni. Kama ilivyo post za watu mitandaoni. Kukamatwa kwake kumefanya kila mtu atake kujua sababu. Alipoambiwa sababu ni wimbo, akataka kujua hiyo sababu ya wimbo ikoje.

Matokeo yake ni kila mtu hata ambaye hana muda na Bongo Fleva akataka kusikiliza. Akasikilizwa. Bao kubwa zaidi ni kitendo cha Rais Magufuli kuufagilia na kuamuru aachiwe na wimbo wake upigwe kila sehemu na aongeze vionjo.

Hii ni bahati ya mtende kuota Jangwani. Ni shangwe na kicheko tu kwa Nay. Hana muda tena wa kupiga simu kwa watangazaji na madj kuwaomba waupige. Ila Kazi inabaki kwao kumsaka Nay kwa ‘intavyuu’ kila siku.

Magufuli ni kama kocha ambaye kamtoa mchezaji uwanjani aliyeanza kukata pumzi na kumuingiza mchezaji kwenda kuziba nafasi yake.

Kasaidia kumeweka kando Darassa ili kumpisha Nay.

Darassa tatizo ni Magufuli siyo Nay.

By Dk Levy, salaamzao@gmail.com , 0744053111

Mwananchi

Comments

comments


Unataka kutangaza nasi? Tumia namba ya simu hapo chini.

Please contact us: email : info@bongomovies.com or Mobile: +255 756 348 364