-->

Gabo: Najengea Daraja la Kuelekea Mafanikio Mawe Tunayopigwa

Dar es Salaam. “Aliyeanzisha virusi kwenye simu, kompyuta, bila shaka alitafuta suluhisho la virusi hivyo akapata tiba yake (anti virus).

“Kwa sababu waigizaji ndiyo chanzo cha kufika hapa filamu zilipo, hatuna budi pia kutafuta suluhisho la tatizo, ” Hivyo ndivyo anavyoanza kueleza mwigizaji Gabo Zigamba.

Gabo Zigamba

Gabo anasema mashabiki wa filamu licha ya kupenda burudani wamechoshwa na mambo yanayotokea katika kazi hiyo iliyokuwa kivutio cha wengi.

Anafafanua kuwa wasanii wamesahau kuwa wanapimwa kwa kile wanachokifanya wakalewa majina jambo ambalo limeifikisha filamu hapa ilipo.

Anasema hataki kuelekeza lawama kwa yeyote miongoni mwao anachotamani kukiona ni kila mmoja kwa wakati wake anatafuta suluhisho la tatizo walilonalo.

“Kuna wanaosema hawaigizi tena, kuna wanaosema soko la filamu limevamiwa, hiyo siyo dawa, tunachotakiwa kufanya ni kufikiria kwa mapana yake nini tufanye ” anasema Gabo.

Gabo anasema kwa kuanza alipata wazo la kukutana na mashabiki kwa muda mfupi popote pale walipo, swali likawa anakutana nao vipi na siku hizi hakuna majukwaa ya kibisa?

Anasema akafanya utafiti mdogo kuona ni kitu gani kinawakutanisha watu wengi kwa wakati mmoja, akabaini ni mitandao ya simu.

“Nikaona hiyo kwangu ni fursa, nikakusanya mawe tunayopigwa kwa pamoja na kujenga daraja kuelekea kwenye mafanikio.

“Hatimaye nakutana na mashabiki wangu kupitia App ya Uhondo, filamu ya “kisogo” ni mwanzo tu zinakuja nyingi kama mvua, mashabiki wake mkao wa kula, ” anasema.

Anasema anavyowafahamu Watanzania wanapenda burudani na kuthamini vya kwao, isipokuwa wanahitaji kilicho bora zaidi ndiyo maana wamewaletea filamu hiyo fupi.

Anaeleza wazo lilikuwa ni kutafuta kuondoa manung’uniko kuhusu Bongo Movie, kwa kufuta makosa na kufanya kitu kitakachowavutia watizamaji na kuleta heshima.

Anasema filamu fupi zitakuwa na mashabiki wengi kutokana na kutotumia muda mwingi wa mtizamaji.

“Mwezi wa saba tunaweza kutizama bure iwapo mambo yatakwenda kama tulivyopanga na ifikapo mwezi wa nane nitaanza kuweka na tamthilia, kidogo kidogo hadi nitafika ninapopataka, ”anasema Gabo.

Anasema dunia imebadilika kuendelea kulaumu na kusubiri dunia irudi nyuma na kufanya vitu vile vile itabaki kuwa ni ndoto, hivyo la maana ni kuangalia jinsi ya kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya teknolojia.

Anafafanua pamoja na manung’uniko ya filamu kuwa na kiwango cha chini, kushuka kwa soko, bado ni ukweli usiopingika kuwa changamoto ya teknolojia inachangia kwa kiasi kikubwa.

Anasema ni ngumu kumlazimisha mtu aende kununua filamu kama hana nafasi hata kama ni nzuri kiasi gani, ilihali muda mchache anaoupata anaweza kufungua simu, kompyuta na kuona filamu zenye kiwango kutoka kila pembe ya dunia.

“Changamoto zipo nyingi, makosa yetu yapo mengi, jawabu la yote ni kujituma, kufikiri upya.

“Inawezekana walikuwa wakishangaa nguo nzuri walizokuwa wakivaa waigizaji hapo nyuma, na wao sasa wanazo, wanahitaji kuonyeshwa kitu kingine watakachoshangaa na kuvutiwa kutizama filamu zetu ” anasema.

By Kalunde Jamal, Mwananchi kjamal@mwananchi.co.tz

Comments

comments


Unataka kutangaza nasi? Tumia namba ya simu hapo chini.

Please contact us: email : info@bongomovies.com or Mobile: +255 756 348 364